Hakuna siku maalum kwa ajili ya
kutafuta mabadiliko, tukiamua siku yoyote tunaweza kubadilika. Siku yoyote
tunaweza kuamua kusoma kitabu ambacho kitakachoifanya akili yako kupata elimu
mpya. Siku yoyote tukiamua tunaweza kuanza na mipango mipya. Tunaweza kufanya
sasa hivi, au wiki ijayo au mwezi ujao, au mwaka ujao.
Vile vile tunaweza tusifanye
kitu chochote. Tunaweza kuendelea kujidanganya kama tunafanya lakini hatuna
tunachokifanya. Na kama mawazo ya kutaka mabadiliko yatatufanya tusiwe na
amani, tunaweza kubaki kama tulivyo. Tunaweza kuchagua chochote lakini tukijipa
sababu tutaishia na kuongea tu. Na kosa halitokuwa la dunia bali ni lako.
Uwezo tunao na wajibu tunao wa
kufanya chaguo bora tutakaloweza kulianza leo. Yeyote anayetafuta maisha
hahitaji majibu zaidi. Hahitaji muda zaidi wa kufikiri ili aweze kufikia
maamuzi.
Hatuwezi kuruhusu makosa
yatuhukumu, yajirudie kila siku na kutuongoza kwenye njia isiyo sahihi.
Lazima tuwe na misingi yote yatakayoleta utofauti mkubwa kwenye maisha.
Kutenda ni mhimili muhimu sana
ambao haustahili kupuuzwa.
Wote wanaotafuta mafanikio na
furaha tayari wametenda kazi nzito. Lakini pia hawakuweza kwenda kuchota tu
hivi hivi. Tatizo ni kwamba ili tuweze kuwa na shauku ya matunda mema ni lazima
tuweke akili, maarifa na nguvu kwenye vitendo vyetu. Kufanya bila ya kutumia
akili na maarifa tunaweza kuharibu. Lakini tusipoteze muda mwingi kwa kutafuta
akili.Vitu hivi huenda kwa makisio na uwiyano.
Ni rahisi kukosea wakati
unapokuwa kwenye mwendo wa mafanikio. Na hii ndio maana kutenda kwetu
tunatakiwa tuwe na mipango kazi. Lakini pia tuwe waangalifu sana ili tuweze
kusonga mbele.
Vitendo vyetu lazima viwe na
mipango. Lazima tutumie maarifa ya kutosha yatakayotuwezesha kupanga mipango
leo kwa lile jambo unalotaka kulifanya kesho. Lazima tuwe na mipangilio ya
baadaye, si tu kulala na kuota.
Kama tutakuwa na nidhamu kwenye
mipango yetu, basi tutakuwa tunajitengenezea bahati mbeleni.
Safari yetu ya mafanikio sio
kama Jumapili au Jumatatu unaamka na kuikuta siku. Hapana lazima tujipange na
tuamue tunataka kuishia wapi. Lazima tuchague kituo na lazima tujiandae
kupambana na changamoto zitakapotokea.
Kwa nini sisi wanaadamu ni
viumbe wenye akili nyingi duniani. Lakini tunaziruhusu akili zetu kuishia
katikati. Kwa nini tusiendelee ili tuweze kupata kile ambacho kinaendana na
thamani yetu.
Sababu ni moja tu ya kwamba
tumejipa uhuru wa kuchagua.
Katika hali nyingi chaguo
linakuja kama zawadi. Lakini zawadi hiyo inapokuja katika hali ya kufanya
kutokana na uwezo wetu, chaguo linabadilika badala ya kuwa neema linakuwa
laana.
Mara nyingi tunachagua kufanya
hafifu kuliko vile ambavyo tungeweza kufanya.
Kuna aina mbili za kuchagua:
Chaguo la kwanza ni kufanya ili
upate kidogo kuliko uwezo wako. Kupata mshahara mdogo,
kufikiri kidogo, kujaribu kidogo, kusoma kidogo, kuwa na nidhamu kidogo. Hili
ni chaguo linalotupelekea tusiwe na mafanikio katika maisha.
Chaguo la pili ni kufanya kwa
uwezo wetu wote kama tunavyostahili kuwa. Kusoma kitabu mwanzo mpaka
mwisho. Kupata zaidi, kufanya zaidi, kutoa na kushirikiana kwa uwezo wetu
wote.
Kwa nini tusichague kufanya kila
kitu tunachoweza kufanya kwa uwezo na akili zetu zote.
Matokeo ndio kipimo sahihi cha
maendeleo yetu. Sio mazungumzo wala maelezo marefu. Na kama matokeo yetu
yamekuwa ya kiwango cha chini kuliko tunavyotarajia, maana yake ni kwamba
tunatakiwa kuweka juhudi zaidi leo kuliko tulivyoweka jana.
Na zawadi kubwa na nzuri siku
zote ipo kwa yule anayeleta thamani kubwa kwake na kwa dunia na kwa wote
waliomzunguka. Na hii inatokana na uchaguzi wake.
Imeandikwa na Ali Khamis,
simu namba 0784498867.
0 comments:
Chapisha Maoni
Asante Sana Na Karibu Tena